Main menu

Pages

INSHA

 

Insha

Kuna aina mbili kuu za Insha.
  • Insha za ubunifu
  • Insha za kiuamilifu
Insha za ubunifu ni insha ambazo mwanafunzi huhitaji kubuni maudhui, mazingira, wahusika, na kadhalika kulingana na swali analorejelea. Insha hizi zinaweza kuwa za methali, mdokezo ama insha zenye mada ambazo hazina mtindo rasmi.

Insha za kiuamilifu ni maandishi yenye mtindo maalum na hutumika katika mazingira halisi kwa kuzingatia mtindo huo rasmi. Kwa mfano kumbukumbu, resipe, barua, ratiba, n.k. Ubunifu wa mwanafunzi hauwezi ukaathiri mtindo wa insha hizi. Kwa hivyo anchohitajika zaidi kuzingatia ni mtindo wa utunzi mada na hoja muhimu.

Insha za Kubuni

Insha za ubunifu ni insha ambazo mwanafunzi huhitaji kubuni maudhui, mazingira, wahusika, na kadhalika kulingana na swali analorejelea. Insha hizi zinaweza kuwa za methali, mdokezo ama insha zenye mada ambazo hazina mtindo rasmi.

Aina za Insha za Kubuni

  1. Insha za Mdokezo
  2. Insha za Methali
  3. Insha za Mada
  1. .

    Insha za Mdokezo

    Hizi ni Insha za ubunifu ambazo mwanafunzi hupewa kifungu cha maneno kinachopaswa kujitokeza katika insha yake.

    Baadhi ya insha za aina hii huwa zimetangulizwa na mwanafunzi hutakiwa akamilishe na nyinginezo huwa na kimalizio. Japo mwanafunzi ana uhuru wa kuiendeleza insha yake atakavyo, ni sharti ajifunge katika maudhui yanayojitokeza katika mdokezo aliopewa. Kwa hivyo, kabla ya mwanafunzi kuiendeleza insha yake, ni sharti atambue maudhui yaliyokusudiwa na mtahini.

    Kwa mfano:

    Endeleza insha ifuatayo na uifanye iwe ya kuvutia:
    1. Nikasikia sauti hiyo tena. Sikuamini masikio yangu. Moyo ukaanza kunienda mbio mbio. Mara upepo....
    2. Giza lilikuwa limechukua milki ya viumbe wote duniani. Nyota zilitoa mwanga hafifu na mwezi ulikuwa ushatua. Katika giza hilo la kaniki....

    au

    Andika insha inayoishia kwa dondoo hili...
    1. ... na kuniacha machozi yakinienda mbilimbili.
    2. ... Hadi wa leo, juhudi zangu za kusahau matukio ya siku hiyo hazifui dafu.

    Insha za Methali

    Methali huwa na pande mbili na ni lazima insha ya methali izipe sehemu zote mbili uzito sawa. Upande mmoja hutoa wazo au pendekezo; na upande wa pili hutoa jibu, suluhisho au matokeo.

    Chukua kwa mfano, "Mpanda ngazi hushuka". Katika insha yako ni lazima utoe hoja za kutosha kuonyesha kwamba mhusika fulani kweli alipanda ngazi (k.v alipata cheo kikubwa, alijisifu n.k). Mwandishi pia anapaswa kutoa hoja za kutosha kuonyesha namna mhusika huyo aliposhuka (k.v akafutwa kazi,n.k) . Kwa mara nyingi, wanafunzi huzingatia tu sehemu ya kwanza ya methali katika insha yote huku sehemu ya pili ikijitokeza katika aya ya mwisho pekee.

    Kumbuka kwamba ni muhimu kuelewa maana ya methali vizuri kabla ya kuchagua insha ya methali.

    Mifano ya Insha za Methali:

    Andika inayoonyesha ukweli wa methali ifuatayo. Ifanye insha yako iwe ya kupendeza.

    1. "Usiache mbachao kwa msala upitao"
    2. "Chururu si ndo ndo ndo"
    3. "Siku za Mwizi ni arobaini"

    Insha za Mada

    Hizi ni insha ambazo mwaandishi hutakiwa kuzungumzia mada fulani kwa kutoa hoja ama maelezo. Insha hizi hazimhitaji mtahiniwa kuanza kusimulia hadithi yake bali ni kurejelea mada aliyopewa. Mwandishi wa insha kama hii anapaswa kuwa na hoja za kutosha kuhusu mada aliyopewa kabla ya kuanza kuiandika. Hoja zote zinapaswa kujitokeza katika masimulizi yenye mtiririko wala si kuorodhesha hoja, moja baada ya jingine.

    Kwa mfano:

    Andika insha juu ya:
    1. Umuhimu wa kupanda miti
    2. Athari za kuavya mimba
    3. Namna ya kuboresha kilimo katika sehemu zenye ukame
    4. Mbinu za kukabiliana na wezi wa mifugo.

    Insha hizi huwa insha halisia na hivyo mwaandishi hawezi kupigia chuku au kutoa hoja zisizo kweli. Kwa mara nyingi insha hizi hurejelea maswala ibuka katika jamii k.v njaa, ukimwi, kilimo, ufisadi, ukabila, n.k

    Hata hivyo mwanafunzi anaweza kupata insha za mada zinazohitaji ubunifu, mapambo ya lugha n.k. Angalia mifano ifuatayo.

    Andika insha juu ya:
    1. "Ndoto Niliyokuwa Nayo"
    2. "Siku Ambayo Sitaisahau Maishani"
    3. "Sherehe Niliyoihudhuria"
    4. "Ajali ya Barabarani Niliyoishuhudia"

    Insha za Kiuamilifu

    Hizi ni insha amabazo huchukua mtindo maalum wa kuandikwa. Japo mwanafunzi anaweza kubuni maudhui katika insha yake, hana uhuru wa kujichagulia muundo atakaotumia kuwasilisha utunzi wake bali anapaswa kuzingatia mtindo maalum wa kuandika insha hiyo.
    Tumekuandalia Insha zifuatazo:
    INSHAMAELEZO KWA UFUPI
    Hotubaandika hotuba kwa hadhira kuhusu mada fulani
    Kumbukumburekodi za mkutano
    Resipeorodha ya viungo na maelekezo ya kuandaa chakula fulani.
    Ratibampangilio wa mambo katika shughuli fulani
    Mazungumzomajadiliano baina ya watu wawili au zaidi
    Mahojianomazungumzo ambapo mtu mmoja anamhoji/kumwuliza maswali mwenzake
    Baruamuundo wa barua rasmi, barua ya kirafiki na barua kwa mhariri
    Taharirimaoni ya mwandishi/mhariri
    Wasifusimulia maisha ya mtu mwengine
    Tawasifusimulia maisha yako mwenyewe
    Mjadalatoa maoni yako kuhusu hoja fulani

    Insha za Barua

    Kuna aina mbili za barua:

    • Barua Rasmi
    • Barua ya Kirafiki

    Pia tutaangalia Barua Kwa Mhariri


    Barua ya kirafiki

    Barua ya kirafiki ni barua ambayo mtu huandika kwa mwenzake au mtu wa familia yake. Barua hii haichukui mtindo wowote maalum wa kuandikwa. Huwa na anuani moja tu: ya mpokeaji. Barua hii haitumii lugha rasmi na mwandishi anaweza kumrejelea mwandikiwa kwa kutumia jina lake la kwanza. Aidha barua za kirafiki haziitaji kutiwa saini.


    Barua Rasmi

    Barua rasmi au barua ya kiofisi/kibiashara huzingatia mtindo rasmi wa barua. Huwa na sehemu zifuatazo:

    Muundo

    1. Anuwani ya mwaandishi huwekwa juu kabisa na huwa katika upande wa kulia wa kartasi.
    2. Tarehe ya barua hiyo - tarehe huandikwa chini ya anwani ya mwandishi
    3. Anuwani ya mpokeaji - Anwani ya anayeandikiwa huwa katika upande wa kushoto wa kartasi, na huwekwa msitari mmoja chini ya tarehe.
    4. Salamu-Chini ya anwani ya mpokeaji, barua huanza kwa kumrejelea mpokeaji kama bwana au bi. Ni makosa kumsalimia mpokeaji wa barua rasmi au kumwuliza hali yake.
      Kwa Bwana Menomakubwa, => taja jina lake ikiwa mnajuana na unayemwandikia.
      Kwa Bw/Bi, => Ikiwa humjui mpokeaji wa barua, tumia bw/bi
    5. Mada -Kichwa cha barua rasmi huja pindi tu baada ya salamu. Hutangulizwa na maneno kama vile KUH:(kuhusu), MINT:(mintarafu). Ni sharti kiachwe kiandikwe kwa herufi kubwa na kipigiwe mstari. Kichwa kinapaswa kuwa kifupi na kinachoelezea mada ya barua kiukamilifu.
    6. Ujumbe - Ujumbe wa barua rasmi lazima uwe mfupi na unaotumia lugha rasmi.
    7. Tamati â€“ mwandishi humalizia kwa maneno ya hitimisho kama vile:
      Wako mwaminifu,

      [jina]

      Sahihi

    Barua kwa Mhariri

    Hii ni barua ya msomaji wa jarida kwa mhariri mkuu wa jarida/gazeti fulani akitoa maoni yake kuhusu jambo fulani kama vile uchumi, kisa, sera za serikali au habari zozote zinazoendelea kwa wakati huo.

    k.m:

    Kwa Mhariri Mkuu

    Jarida la Mwenda Zake Leo

    MINT : HATUA YA SERIKALI KUFADHILI SEKTA YA BODABODA



    ...ujumbe...

    Na [jina]

Hotuba

Insha ya hotuba ni insha ambayo hutoa maneno halisi ya mzungumzaji/hatibu/kiongozi anapozungumzia hadhira, kuhusu jambo fulani. Insha ya hotuba huandikwa katika hali ya usemi halisi na mwandishi hatakiwi kuweka alama za kunukuu anapoanza insha yake.

Hotuba inaweza kutolewa na kiongozi wa kisiasa, utawala, kidini, kikundi, shirika fulani, daktari, n.k. Hadhira katika hotuba husheheni wageni waalikwa, wanachama, wafuasi, wananchi, n.k ambao wanahusishwa katika mada inayorejelewa katika hotuba hiyo. Mengi ya maswala yanayojitokeza katika insha za hotuba ni maswala ibuka katika jamii k.v upangaji wa uzazi, usalama, n.k

Muundo wa Hotuba

  1. Anwani

    Anwani, mada au kichwa cha hotuba huchukua herejelea hatibu pamoja na mada ya hotuba. Pia mada inaweza kutaja hadhira.

    • Hotuba ya Waziri wa Afya kuhusu madhara ya ukimwi kwa wananchi.
    • Hotuba ya Mwalimu Mkuu kwa Wazazi
  2. Utangulizi

    • Anza hotuba yako kwa kuwatambua waliohudhuria mkutano (hadhira).
    • Wataje kwa majina/vyeo vyao kuanzia yule wa cheo cha juu hadi wa chini, mabibi na mabwana. Kumbuka kwamba hauhitajiki kuwasalimia. Kuwatambua kwa majina pekee kunatosha.
    • Jitambulishe kwa hadhira yako hasa ikiwa unazungumzia hadhira isiyokujua au wageni.
    • Tanguliza mada yako. Kwa mfano:
      Waziri wa Kilimo, Mkuu wa Wilaya, Chifu wa Kisioni, wanachama wa kikundi hiki cha Rotuba Bora, mabibi na mabwana. Ni matumaini yangu kwamba nyote mu buheri wa afya. Mimi ni mwakilishi wa Kikundi cha Mshipi wa Kijani Kibichi na jioni ya leo kuna jambo muhimu ambalo ningependa sote tulifahamu ili kuboresha mazingira yetu kwa ...
  3. Mwili

    • Hakikisha kuna mtiririko wa hoja kuanzia mwanzo hadi mwisho
    • Ujumbe wako wote unapaswa kuwa katika usemi halisia wala si wa taarifa.
  4. Tamati

    • Hakikisha kwamba mwisho wa hotuba yako unatambulika.
    • Unaweza kumaliza kwa shukurani

Mfano ya Insha za Hotuba:

  1. Wewe ni chifu katika kijiji cha Kikanyageni. Andika hotuba utakayotoa kwa vijana kuhusu hatua za serikali kukabiliana na matumizi ya dawa za kulevya.
  2. Umealikwa kuwahutubia wanafunzi wa shule ya msingi uliyosomea kuhusu umuhimu wa elimu ya wasichana. Andika hotuba utakayotoa.
  3. Wewe ni daktari. Andika hotuba utakayotoa kuwahimiza wanawake wakubali kutumia mbinu za kupanga uzazi.
  4. Umeteuliwa na afisa katika idara ya utalii kuhutubia watalii kuhusu changamoto za kiusalama zinazolikabili bara hili na upendekeze mbinu za kuzitatua.

 Insha za Kumbukumbu

Kumbukumbu za mikutano ni rekodi zinazowekwa na katibu wa mkutano mkutano unapoendelea ili kuhifadhi yanayojadiliwa na kukubalianwa katika mkutano huo. Katibu anapaswa kufuatilia mtindo maalum wa kuandika kumbukumbu hizo kulingana na mpangilio katika mkutano.

Muundo wa Kumbukumbu

1. Kichwa cha kumbukumbu

Kichwa cha kumbukumbu kinapaswa kutaja mambo yafuatayo:
  • Ni mkutano wa akina nani?
  • Unaandaliwa wapi?
  • Unaandaliwa lini?
  • Unaanza saa ngapi?
Mfano wa Kichwa cha Kumbukumbu:
Kumbukumbu za Mkutano wa Shirika la Msalaba Mwekundu Shuleni ulioandaliwa tarehe saba Agosti 2001 katika Ukumbi wa Mikutano kuanzia saa Tisa alasiri.

2. Waliohudhuria

Andika orodha ya wote waliofika kwenye mkutano huku kuanzia na yule mwenye cheo cha juu zaidi hadi kwa wanachama. Pia onyesha vyeo vyao.

3.Waliotoa Udhuru

Hawa ni wale walioomba ruhusa kutohudhuria mkutano ====

4.Waliokosa kuhudhuria

Hawa ni waliokosa kuhudhuria mkutano, bila kutoa udhuru)

5.Waalikwa

Hawa ni wageni walioalikwa katika mkutano, k.v mlezi wa chama, afisa wa kiutawala, n.k)

6. Ajenda

Orodhesha hoja zitakazorejelewa katika mkutano huo
KUMB 1kumbukumbu ya kwanza huwa ni kufunguliwa kwa mkutano na ujumbe kutoka kwa mwenyekiti.
KUMB 2Kusomwa kwa kumbukumbu za mkutano uliotangulia na kuthibitishwa kwa kumbu kumbu hizo kwa kutiwa saini.
KUMB 3Maswala yanayoibuka kutokana na kumbu kumbu zilizosomwa. (Kumbuka kutaja nambari ya kumbu kumbu hizo)
KUMB 4 kuendeleaMaswala katika ajenda
KUMB ya MwishoMaswala mengineyo yasiyokuwa kwenye orodha ya ajenda.
Tamatikufungwa kwa mkutano. Taja mkutano ulifungwa saa ngapi; mkutano ujao utakuwa tarehe ngapi; kisha acha nafasi ya kuthibitishwa kwa kumbu kumbu hizo katika mkutano utakaofuatia.

Mfano wa Insha ya Kumbukumbu

KUMBUKUMBU ZA MKUTANO WA CHAMA CHA KISWAHILI ULIOANDALIWA KATIKA CHUMBA CHA MIJADALA TAREHE 2 APRILI 2010 KUANZIA SAA TATU ASUBUHI

Waliohudhuria

  • Thoma Mwororo - Mwenyekiti
  • Vivian Mjaliwa - Mweka hazina
  • Idi Baraka - Mkuu wa utafiti
  • Fikra Mawimbi - mwanachama
  • Mercy Rehema - katibu

Waliotuma Udhuru

  • Bahati Sudi - Naibu Mwenyekiti
  • Paul Kitanzi - Msimamizi wa Mijadala

Waliokosa Kuhudhuria

  • Zakayo Chereko - Spika
  • Juma Mtashi - mwanachama

Waalikwa

  • Mdaku Mpelelezi - Mwanahabari
  • Bw. Msawali - Mlezi wa Chama
Ajenda
  • Uchapishaji wa jarida la Kiswahili
  • Shindano la kuandika insha.
  • Kusajili wanachama wapya

KUMBUKUMBU 1/04/10 - KUFUNGULIWA KWA MKUTANO

Mwenyekiti aliwakaribisha wanachama wote na baada ya kuwatambulisha wageni, akawaomba washiriki wawe huru kuchangia katika ajenda mkutano huu ili kuboresha chama.

KUMBUKUMBU 2/04/10 - KUREJELEA KUMBUKUMBU ZA MKUTANO ULIOPITA.

Katibu alisoma kumbukumbu za mkutano wa mwezi Machi. Kumbukumbu zilikubaliwa na wanachama wote na kuthibitishwa na mwewnyekiti pamoja na katibu kwa kutia saini.

KUMBUKUMBU 3/04/10 -MASWALA IBUKA KUTOKANA NA KUMBUKUMBU ZILIZOSOMWA

Mweka hazina alifahamisha mkutano kwamba aliongea na mkuu wa idara ya Kiswahili kuhusu ufadhili kama tulivyokuwa tumekubaliana katika KUMB 9/03/10 ya mkutano uliopita.

KUMBUKUMBU 5/04/10 - HAFLA YA KISWAHILI

Iliripotiwa kwamba hafla ya Kiswahili ambayo wanachama walikuwa wamealikwa kuhudhuria katika Shule ya Sakata Academy haingeweza kufanyika kutokana na tamasha za muziki zilizokuwa zinaendelea katika shule hiyo. Wanachama waliokuwa wamejitayarisha kwa mashairi waliombwa kuendelea kujifunza ili wayawasilishe muhula wa pili.

KUMBUKUMBU 4/04/10 - UCHAPISHAJI WA JARIDA LA KISWAHILI

Wanachama walikubaliana:-
  • Kwamba chama kitaanza kuchapisha jarida la Kiswahili
  • Kwamba jarida litakuwa likichapishwa mara moja kila muhula na kuuzwa shuleni
  • Kwamba kila mwanachama atachangia katika kuandika makala na kuuza nakala za jarida hilo.
  • Kwamba paneli ya wahariri lingeundwa ili kuongoza idara ya uchapishaji
  • Kwamba hazina ya chama ina fedha za kutosha kuzindua uchapishaji huo.

KUMBUKUMBU 5/04/10 - SHINDANO LA KUANDIKA INSHA

Kila muhula wa pili, chama huandaa shindano la kuandika insha ambalo wanafunzi wote hushiriki. Insha zilizopendekezwa mwaka huu ni:-
  • "Jadili chanzo cha migomo shuleni na namna ya kusuluhisha."
  • ... ... ... ... ... ... ... ... ...
  • ... ... ... ... ... ... ... ... ...
  • ... ... ... ... ... ... ... ... ...

KUMBUKUMBU 6/04/10 KUSAJILI WANACHAMA WAPYA

... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ...

KUMBUKUMBU 7/04/10 MASWALA MENFINEYO

... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ... ...

KUFUNGWA KWA MKUTANO

Mkutano ulifungwa saa kumi na nusu, baada ya maswala yote kujadiliwa. Mkutano unaofuatia ulipoangwa kuwa tarehe ishirini mwezi Mei, katika Ukumbi wa Muziki.

KUTHIBITISHWA KWA KUMBU KUMBU

___________________________
MwenyekitiKatibu
Tarehe:________Tarehe:________
Tanbihi: Usitie saini. Sahihi itawekwa katika mkutano ufuatao

Insha za Mahojiano

Hizi ni insha ambazo mhusika mmoja huwa akimhoji au kumwuliza maswali mwenzake.

  1. Mahojiano ya mtu anayeomba kazi
  2. Mahojiano baina ya askari na shahidi kuhusu kisa cha mauaji
  3. Mahojiano baina ya mwaandishi wa habari na mwananchi kuhusu katiba mpya
  4. Mahojiano baina ya daktari na mgonjwa

Insha za Mazungumzo au Majadiliano

Hii ni insha ya mazungumzo baina ya watu wawili au zaidi. Ni lazima wahusika katika mazungumzo wajitokeze vizuri na sifa zao zitambulike. Hatutarajii watu katika mazungumzo wawe na fikira moja na usawa katika mapendekezo yao. Ukinzani au tofauti ya uteuzi wa maneno kati ya usemi wa mzungumzaji mmoja na mwengine ni lazima ijitokeze.

Mazungumzo yanaweza kuwa ya kutafuta suluhisho baina ya pande mbili zinazozozana kama vile mama na bintiye; kupanga jambo fulani, n.k

Insha ya Mazungumzo huandikwa katika usemi halisia, huku wasemaji wakionyeshwa kama vile mchezo wa kuigiza.

Vitendo vya wahusika huonyeshwa kwa mabano

Mfano wa Insha ya Mazungumzo

Mazungumzo baina ya Mwalimu Mkuu, Mwanafunzi na Babake kuhusu nidhamu ya mwanafunzi huyo.

Mwalimu:Bwana Juma, nimekuita umchukue mtoto wako ukamsomeshe katika shule nyingine kwa maana amtushinda sisi.
Mzazi:Ikiwa amewashinda na ninyi ndio mlio na kiboko, si ataniua mimi! Hata mimi simtaki kwa maana simwezi. Hawezi kuja kwangu
Juma:Nimesema sitaki kusoma! Nimechosha na mtindo huu…
Mzazi:(akikunja shati)... ...


Insha za Mjadala

Insha ya mjadala humhitaji mwanafunzi atoe maoni yake kuunga mada na pia kupinga kauli fulani. Katika insha za aina hii, mwanafunzi anaweza kuegemea upande mmoja tu ikiwa upande wa kupinga hauna hoja za kutosha.


Ratiba

Ratiba ni orodha ya mpangilio wa namna mambo yatakavyofuatana katika shughuli fulani. Lengo lake ni kuhakikisha wakati unatumiwa vizuri ili mambo fulani yasije yakakosa kutendwa kutokana na upungufu wa wakati.

Ratiba hutumika katika sherehe, mikutano, mazishi, hafla, tamasha, n.k


Sehemu za Ratiba

  1. Kichwa

    Kichwa cha ratiba hutaja mambo yafuatayo:
    1. Shughuli yenyewe - Taja jina la tukio ambalo unaandalia ratiba. Kwa mfano Harusi ya Bwana na Bi Arusi, Siku ya Zawadi
    2. Tarehe ya shughuli - je shughuli hiyo itafanyika lini?
    3. Mahali- Taja mahali ambapo shughuli hiyo itafanyikia. kwa mfano katika uwanja wa michezo wa Kasarani, kanisa la St. Mtakatifu
    Mfano wa kichwa cha ratiba:
    • Ratiba ya Hafla ya Ukimwi katika Bustani la Uhuru tarehe tano Januari.
    • Ratiba ya Mazishi ya Dkt. Marehemu tarehe 20/12/1923 Kijijini Vikwazoni
  2. Mwili

    Mwili wa ratiba hujumuisha mambo mbalimbali yatakayofanyika katika mpangilio maalum, saa mbalimbali. Ni vizuri kuzingatia vipengele vifuatavyo:
    1. Saa - Onyesha saa ambazo tukio limepangiwa kuanza hadi linapotakiwa kumalizika
    2. Mahali - Ikiwa shughuli tofauti zinafanyika katika mahali mbalimbali kama vile vyumba tofauti, inapaswa hutaje mahali ambapo kila jambo litafanyikia.
    3. Wahusika - Taja mtu au watu waliopewa wajibu wa kutekeleza jambo fulani. Hii huwasaidia kujitayarisha ipasavyo.

Mfano wa Ratiba

RATIBA YA MAZISHI YA MZEE MAUTI TAREHE 20/12/1923 KIJIJINI MIZUKANI

SAASHUGHULI
07: 00Marafiki wa Mauti watoa mwili kutoka SlowDeath Hospital
10: 30Maombi katika kanisa la G.I.Z.A yakiongozwa na Pst. Muna Fiki
11: 15Mwili kuwasilishwa nyumbani, familia ya Mauti
12: 00Kupakuliwa kwa chakula na Bi Kamafisi, Bi Mwachafu na wapishi walioteuliwa
1: 10Kukusanyika kwa umati
2: 00Maombi ya kuanzisha shughuli za mazishi
2: 30Shuhuda zikiongozwa na Mzee Siachwinyuma
3: 00Ushuhuda wa serikali na Chifu Mtesi
3: 40Kuteremshwa kwa mwili kaburini na vijana walioteuliwa
4: 00Shukrani za Mwisho, na Mwenyekiti wa Chama cha Kufa Tukusaidie
6: 00Kugawana mali ya marehemu, na wazee wa kijiji

Resipe

Haya ni maandishi yanayotoa maagizo/maelekezo ya kuandaa chakula fulani.


Sehemu muhimu za resipe ni:

  1. Kichwa- Jina la mlo unaoandaa, Idadi ya watu wanaopikiwa
  2. Orodha ya viungo unavyohitaji- majina ya viungo, Idadi au kiasi kinachohitajika
  3. Maagizo/namna ya kupika
  4. Eleza kwa utaratibu kila hatua
  5. Taja wakati utakaotumika katika kila hatua.
  6. Hakikisha kila aina ya viungo ulivyotaja, inajitokeza katika maelezo ya kupika.
  7. Tamati
  8. Baada ya chakula kuiva, eleza kinaweza kupakuliwa na chakula kipi kinginecho k.v ugali na kitoweo cha kuku

Mfano

  1. Andika resipe ya kuandaa mchuzi wa kuku kwa watu watano.
  2. Andika resipe ya kuandaa chakula kwa mgonjwa wa moyo

Tahariri

Tahariri ni makala ya mhariri (mkuu) wa jarida/gazeti fulani. Mhariri mkuu hutoa maoni yake kuhusu mojawapo ya maswala ibuka. Sehemu kuu za tahariri ni:

  1. Jina la Gazeti/jarida
  2. Tarehe/nambari ya toleo hilo
  3. Mada ya Tahariri
  4. Ujumbe
  5. Jina la mwaandishi

Wasifu

Wasifu ni insha inayosimulia maisha ya mtu fulani tangu kuzaliwa kwake, elimu yake, kazi, ujuzi wake n.k. Anayeandika wasifu ni tofauti na anayezungumziwa katika wasifu huo.

Kuna aina tatu za wasifu:

  • Wasifu wa Kawaida
  • Tawasifu
  • Wasifu-Kazi

Wasifu

Wasifu wa kawaida ni masimulizi ya maisha ya mtu fulani yanayosimuliwa na mtu mwengine. Kwa mfano, Wasifu Wa Siti Binti Saad ulioandikwa na Mwalimu Shaaban Robert.
Katika insha, mwanafunzi anawezaambiwa aandike wasifu wa:

  • mtu mashuhuri- anayejulikana kama vile Nelson Mandela, Julius Nyerere au Mzee Jomo Kenyatta n.k
  • mtu yeyote anayemjua - kama vile mzazi, rafiki, somo(kielelezo), mwalimu wake n.k
  • mtu wa kubuni - mwanafunzi anaweza kubuni mtu na asimulie maisha yake

Tawasifu

Katika tawasifu, mwandishi huwa anasimulia maisha yake mwenyewe. Hivyo basi, tawasifu huandikwa na kusimuliwa katika nafsi ya kwanza.
Katika insha, mwanafunzi anaweza ulizwa asimulie:

  • maisha yake binafsi
  • maisha yake, miaka kadhaa ijayo
  • maisha ya mtu fulani kama yake binafsi k.m ajifanye kuwa Rais wa Tanzania, halafu asimulie maisha yake tangu kuzaliwa hadi alipo. k.m 'Umekuwa Rais wa nchi yako kwa muda wa miaka mitano, andika tawasifu kuhusu maisha yako itakayowasaidia wananchi wako kukuelewa vyema zaidi
  • maisha ya mhusika wa kubuni, kama yake binafsi
Kwa mfano, katika riwaya ya Siku Njema, mhusika Kongowea Mswahili anaandika tawasifu akisimulia maisha yake tangu kuzaliwa, maisha ya nyumbani, elimu yake, kazi alizozifanya, maono yake n.k

Wasifu-Kazi

Wasifu-kazi (Resume/Curriculum Vitae) ni stakabadhi inayotumiwa kuorodhesha mambo muhimu katika maisha ya mtu kama vile elimu, kazi, ujuzi n.k inayotumiwa sanasana katika kuomba kazi. Kinyume na wasifu na tawasifu ambazo hutumia lugha natharia (ya masimulizi), wasifu-kazi hutumia muundo fulani wa orodha na/au jedwali kuwasilisha mambo muhimu tu. Isitoshe, wasifu kazi huwa fupi - aghalabu ukrasa mmoja.

Tunapoorodhesha mambo fulani katika wasifu, tunaanza na yale ya hivi karibuni hadi yale ya kitambo. Kwa mfano, anza na shule uliyosomea mwisho, iliyokuwa imetangulia hiyo n.k hadi shule uliyoenda kwanza.

Muundo wa Wasifu-Kazi

Katika wasifu-kazi unahitajika kuonyesha:
  1. Jina lako
  2. Namna ya mawasiliano (simu, anwani, barua pepe)
  3. Elimu
    • orodhesha shule zote ulizozisomea kutoka shule uliyosomea mwisho hadi shule ile uliyoihudhuria kwanza.
    • katika kila shule, onyesha miaka uliyohudhuria k.m 1996-2000
    • onyesha shahada (degrees) na diploma ulizozipata
  4. Kazi
    • orodhesha kazi zote ulizozifanya kutoka kazi ya hivi karibuni hadi kazi ulizozifanya mwanzoni
    • onyesha cheo ulichokuwa nacho katika kazi hiyo na majukumu yake
    • onyesha kampuni au mahali ulipofanya kazi hiyo
    • onyesha miaka ambayo ulikuwa katika kazi hiyo
    • taja ujuzi au taaluma uliyoipata katika kazi hiyo
  5. Ujuzi / Taaluma - taja ujuzi maalumu ulionao, taaluma au talanta zozote zinazokufanya
  6. Mapato/Mafanikio/Tuzo - taja mafanikio yoyote au tuzo zozote ulizozipata katika maisha
  7. Mapendeleo - Nini kinakupendeza katika maisha? unapenda kutumiaje muda wako wa likizo usiokuwa wa kazi
  8. Maono ya Kazi - una maono gani katika kufanya kazi? ungependa kufanya nini?

Angalia hapa baadaye kwa mfano wa wasifu-kazi.

Comments

KISWAHILI REVISION PAPERS

KISWAHILI PP1 KCSE PAST PAPERS KISWAHILI MASWALI paper 1 MS KCSE PAST PAPERS KISWAHILI MASWALI paper 2 MS KCSE PAST PAPERS KISWAHILI MA…

Image